Thursday, July 21, 2011

JK atoa ufafanuzi kuhusu barabara Serengeti

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatano, Julai 20, 2011, ametumia siku ya pili ya ziara yake ya kihistoria katika Afrika Kusini kwa kutembelea na kushawishi wawekezaji wa kilimo cha zabibu na utengenezaji divai kutoka nchi hiyo kuwekeza katika kilimo cha zao hilo mkoani Dodoma.

Aidha, Rais Kikwete ametembelea Kisiwa cha Robben, kilichoko kilomita 12 kutoka mjini Cape Town ambako viongozi wakuu wa mapambano ya kupinga siasa za ubaguzi wa rangi za makaburu walifungwa kwa vipindi kirefu wakiwemo marais watatu kati ya wanne walioongozwa Afrika Kusini tokea Uchaguzi Mkuu wa Kidemokrasia wa mwaka 1994 – Waheshimiwa Nelson Mandela, Kgalema Mothlante na Jacob Zuma.

Rais mwingine ambaye ameongoza Afrika Kusini tokea wakati huo, Mheshimiwa Thabo Mbeki hakufungwa katika Kisiwa hicho lakini baba yake hayati Govin Mbeki alifungwa na akina Mandela kwenye Kisiwa hicho.

Rais Kikwete akifuatana na Mama Salma Kikwete na ujumbe wake ametumia siku ya pili ya ziara yake ya kidola katika Afrika Kusini kutembelea mashamba ya zabibu na kiwanda cha kutengeneza divai katika Jimbo la Cape Magharibi ambalo mji wake mkuu ni Cape Town.

Rais Kikwete amewasili kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Cape Town asubuhi ya leo akitokea Pretoria na kwenda moja kwa moja kutembelea Kisiwa cha Robben ambako alitembezwa kwa kiasi cha dakika 40 kabla ya kuelekea kwenye shamba na kiwanda cha kupanda zabibu na kutengeneza divai la Waterford Estate lililoko katika eneo la StellenBosch, eneo maarufu kwa zao la zabibu na utengenezaji wa divai.

Akizungumza na wenye kiwanda cha Waterford, Rais Kikwete amewaomba kufikiria kwa makini uwezekano wa kuwekeza katika mashamba ya zabibu na utengenezaji divai kwa kushirikiana na wakulima wadogo wadogo wa eneo la Dodoma.

“Naomba mfikirie kwa makini kabisa ombi langu la kuwataka mje kuwekeza katika kilimo cha zabibu na utengenezaji divai kwa kushirikiana na wakulima wa Mkoa wa Dodoma. Katika mkoa huu, zabibu huvumwa mara mbili kwa mwaka tofauti na nchi nyingine duniani na wakulima katika eneo hilo wanaweza kunufaika na ujuzi na uzoefu wenu na kuwapandia zabibu kwa ajili ya kuendesha kiwanda chenu,” Rais Kikwete amewaambia wakulima hao.

Kiwanda cha Waterford kilianzishwa Aprili mwaka 1998 na familia mbili ambazo ni ile ya Jeremy na mke wake Leigh Ord pamoja na ile ya Kevin Arnold ambaye ni mtengenezaji divai pamoja na mkewe.

Kiwanda hicho ambacho kwa sasa kinatengeneza kiasi cha masanduku 35,000 ya divai kwa mwaka ikiwa ni divai nyekundu na nyeupe ni moja ya viwanda vinavyoongoza katika Afrika Kusini kwa kutengeneza divai bora duniani.

(Att. Media: Kurugenzi ya Mawasiliano leo, Alhamisi, Julai 22, itatoa Makala Maalum kuhusu ziara ya Mheshimiwa Rais Kikwete katika Kisiwa cha Robben).


Imetolewa na:

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais,
Safarini, Pretoria
Afrika Kusini

No comments: