JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
BUNGE LA TANZANIA
Simu Na. 022 2112065/7
Fax Na. (255) 022 2112538
E-mail: tanzparl@parliament.go.tz mailto:ParlDom@bunge.go.tz
S.L.P. 9133
DAR ES SALAAM
TAARIFA KWA UMMA
YA: UFAFANUZI KUHUSU HABARI YA GAZETI LA TANZANIA DAIMA LA
TAREHE 5/9/2011 ILIYOSEMA “UCHUNGUZI UDA KUANZA LEO”
Katika Gazeti la Tanzania Daima la tarehe 5 Septemba 2011 lilichapisha
habari yenye kichwa kilichosomeka “Uchunguzi UDA kuanza leo” ikieleza
kuwa kamati iliyoundwa na Bunge kuchunguza kashfa ya uuzwaji wa Shirika
la Usafiri Dar es salaam (UDA) ilitarajia kuanza kazi yake siku ya Jumatatu 5
Septemba 2011 chini ya uwenyekiti wa Mhe. Murtaza Mangungu, Mbunge wa
Kilwa Kaskazini CCM.
Ofisi ya Bunge inapenda kutoa taarifa kwa vyombo vya Habari na Umma kwa
ujumla kuwa taarifa hiyo ni potofu na haina ukweli wowote. Ukweli ni
kwamba mpaka sasa hakuna kamati yoyote ya Bunge inayochunguza suala la
uuzwaji wa Shirika la Usafiri Dar es salaam (UDA). Ikumbukwe kwamba
wakati wa Bunge la Bajeti, Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya
Umma Mhe. Zitto Kabwe (Mb) aliongea na waandishi wa Habari kuhusu nia ya
Kamati yake kufanya uchunguzi huo ikiwa ni pamoja na mapendekezo ya
wajumbe aliyowasilisha kwa Mhe. Spika kwa lengo la kupata kibali chake kwa
muibu wa Kanuni za Bunge.
Aidha, ifahamike kuwa uamuzi wa Mhe.Spika kuhusu suala hilo ulikuwa ni
kuliacha lichunguzwe na Mdibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali
(CAG) na baadae CAG awasilishe taarifa ya uchunguzi wake Serikalini na
hatimaye Bunge liarifiwe matokeo ya Uchunguzi huo kupitia Serikali
Hata hivyo ieleweke kuwa, Kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge,
Toleo la 2007, Kanuni ya 117, inaeleza kuwa Bunge linaweza kuunda Kamati
Teule kwa madhumuni maalumu kwa hoja Mahususi itakayotolewa na
Kuafikiwa Bungeni. Na fasili ya (4) inasema kuwa wajumbe wa kamati Teule
watateuliwa na Spika na watamchagua Mwenyekiti wa Kamati hiyo kutoka
miongoni mwao. Pili, kanuni ya 114 (3) inatamka bayana kuwa kamati ya
kudumu itakutana kila inapoitwa na Spika, Naibu Spika au na Mwenyekiti
wake baada ya kupata idhini ya Spika
Mwandishi wa habari hiyo, hakufuatilia uhalali wa kile alichokusudia kuandika
na hata kujiridhisha na utaratibu wa kamati zinavyofanya kazi kwa mujibu wa
kanuni na badala yake aliandika maoni yake kwa jinsi alivyohisi. Hili ni jambo
la hatari!
Mwisho, tunapenda kuwakumbusha waandishi wote wa Habari kuzingatia
miiko ya kazi yao na kuwa makini waandikapo jambo lolote kwa wasomaji
wao, kwani wasipofanya hivyo na kuandika habari za kupotosha,
wanasababisha usumbufu usio wa lazima na wanaweza kulaumiwa
kusababisha mikanganyiko miongoni mwa jamii yetu.
Ofisi ya Bunge inapenda kuwaarifu wananchi wote wakiwemo wanahabari
kuwa Idara yake ya Habari imekuwa ikitoa na itaendelea kutoa ushirikiano wa
kutosha kuwaarifu waandishi kuhusu taarifa zozote wanazohitaji na hususani
wanazotaka kuandikia habari. Aidha, tunasikitishwa na uandishi wa namna hii
wa kuandika kwa kutegemea hisia bila hata kufanya jitihada za kutosha za
kuwasiliana na Ofisi ya Bunge.
Ofisi ya Bunge iko wazi kutoa ushirikiano kwa ufafanuzi wowote
utakaohitajika.
Imetolewa na:
Idara ya Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa
Ofisi ndogo ya Bunge
Dar Es Salaam
8 Septemba 2011
No comments:
Post a Comment